Kamandi ya Jeshi la Akiba

Jeshi la Akiba lilianzishwa mwaka 1965 kama sehemu ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Uanzishwaji wa Jeshi hili una hadhi ya kisheria kupitia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kifungu Na. 147 (1) (2), Reserve Force Act Na. 2 ya mwaka 1965 na sheria ya Ulinzi wa Taifa Na. 24 ya mwaka 1966 ibara ya 10. (1) (b) - (d). Jeshi hili liliundwa kwa lengo la kuandaa nguvu ya akiba kwa ajili ya kusaidiana na Jeshi la kudumu JWTZ na vyombo vingine vya usalama katika kudumisha Ulinzi na Usalama wa nchi yetu.

Shughuli za Jeshi la Akiba zilikuwa zikiratibiwa na Tawi la Jeshi la Akiba Makao Makuu ya Jeshi. Mwanzoni Tawi hili lilijulikana kama Tawi la Mgambo. Mwaka 2010 kulifanyika mabadiliko ya Muundo Makao Makuu ya Jeshi ambapo Tawi la Mgambo lilibadilishwa jina na kuitwa Tawi la Jeshi la Akiba. Aidha, Halmashauri ya Majeshi ya Ulinzi katika kikao chake cha tarehe 16 Jul 13 ilijadili na kukubaliana uanzishwaji wa Kamandi ya Jeshi la Akiba (KJA) “Reserve Forces Command” .

Waziri wa Ulinzi na JKT kwa Mamlaka aliyopewa chini ya kifungu cha 10 (2) cha Sheria ya Ulinzi wa Taifa alianzisha Kamandi ya Jeshi la Akiba tarehe 08 Disemba 2014.

DIRA NA DHIMA YA KJA

DIRA

Kuwa Kamandi ya Jeshi la Akiba yenye Uwezo wa Kutekeleza dhana ya Ulinzi wa Taifa Kuwa Jukumu la kila Mtanzania (Umma).

DHIMA

Kuwa Kamandi ya Jeshi la Akiba yenye Uwezo wa kuandaa nguvu ya akiba kwa ajili ya kusaidiana na Jeshi la Kudumu (Regular Force) na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama katika kudumisha Usalama wa Nchi yetu.