Mashindano haya yalianzishwa rasmi mwaka 2014. Lengo la mashindano haya ni kudumisha mshikamano, kuvumbua na kukuza vipaji, pia mashindano hayo yatatumika katika kuteua kombaini ya timu ya JWTZ itakayowakilisha Jeshi na Taifa kwa ujumla katika mashindano ya michezo ya Majeshi na utamaduni kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo mwaka huu 2017, yanatarajiwa kufanyika nchini Burundi baadaye mwezi wa nane.
Kauli Mbiu ya mashindano haya ni, “Tushiriki Michezo kama sehemu ya Kazi, Kulinda Afya zetu na kudumisha mshikamano”. Michezo ni furaha na zaidi michezo inakuza nidhamu pamoja na kujenga afya ya mwili na akili kwa Wanajeshi.
Timu zinazoshiriki mashindano haya ni Ngome (Makao Makuu JWTZ), Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Kamandi ya Jeshi la Anga, Kamandi ya Jeshi la Wanamaji pamoja na Jeshi la Kujenga Taifa(JKT).
Mashindano haya yanahusisha michezo ifuatayo; Mpira wa miguu kwa Wanaume, Mpira wa kikapu kwa Wanaume, Mpira wa mikono kwa Wanaume, Mpira wa pete kwa Wanawake, Mpira wa wavu kwa Wanawake na Mbio za nyika kwa Wanaume na Wanawake. Michezo hii inafanyika katika Viwanja vya Twalipo vilivyopo Mgulani pamoja na Uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.
Mwaka huu mashindano haya yamefunguliwa rasmi tarehe 26 Mei 2017, katika Uwanja wa Uhuru na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe (Mb),. Aidha, Mashindano haya yanatarajiwa kufungwa rasmi tarehe 06 Juni 2017.
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.