Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance Mabeyo leo tarehe 17 Disemba, 2020 amezungumza na Maafisa na Askari wa Kikosi cha Ndege za Usafirishaji kilichopo Ukonga jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kikosini hapo Jenerali Mabeyo aliwapongeza Maafisa na Askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kutekeleza majukumu yao kwa weledi hasa katika kipindi cha uchaguzi mkuu wa 2020, kwani uchaguzi umeisha salama na kuwataka kuendelea kuchapa kazi kwa bidii huku wakikumbuka viapo vyao kila wanapokuwa wakitekeleza majukumu yao.
Aidha, amesema kuwa mafanikio tulioyapata ni matokeo ya kufanya kazi kwa upendo, ushirikiano, utii, uadilifu na kujituma. Jenerali Mabeyo amesisitiza kuwa kwa kufanya hivyo tutakuwa tunawahakikishia wananchi kuwa Taifa lipo salama na waendelee kufanya shughuli zao ili kujiletea maendeleo binafsi na Taifa kwa ujumla.
Alisisitiza kuwa Wanajeshi wanapaswa kutojihusisha na masuala ya kisiasa na udini kwani vinaweza kuligawa Jeshi na kupelekea uwepo wa makundi na kuondoa umoja uliopo.
Kuhusu ugonjwa wa Corona, Mkuu wa Majeshi amewataka Maafisa, Askari na Familia zao kuendelea kuchukua tahadhari juu ya ugonjwa huo. " Tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezimungu kwani yapo Mataifa mengi yameathirika na ugonjwa huu, lakini sisi ametuepusha na janga hili" alisema Mkuu wa Majeshi.
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.