Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 22 Machi 2021 ameongoza maelfu ya watanzania jijini Dodoma na mikoa jirani katika siku ya tatu ya kuuaga mwili wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Hafla hiyo imefanyika katika uwanja wa Jamhuri jijini humo.
Shughuli hizo zimefanyika kitaifa jijini humo ambapo zilipambwa na gwaride rasmi lililoandaliwa na Maafisa, Maafisa Wanafunzi na Askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Aidha sherehe hizo zilihudhuriwa na marais kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kenya, Msumbiji, Visiwa vya Comoro, Zimbabwe, Zambia, Malawi, Afrika Kusini na wawakilishi kutoka katika nchi za Burundi, Rwanda na Namibia.
Viongozi hao walipata fursa ya kutoa salamu za rambirambi na kuwataka Watanzania kuendelea kuwa watulivu, na kudumisha amani iliyopo nchini. Rais wa Kenya na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Mhe. Uhuru Kenyatta aliwataka Watanzania kumpa ushirikiano Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake cha uongozi wake ili kuweza kuyakamilisha yale yote yaliyoachwa na mtangulizi wake.
Akizungumza na Watanzania, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan aliwatoa hofu Watanzania kwa kuwahakikishia kuwa yeye atayaendeleza yale yote ambayo ameyaacha mtangulizi wake kwa maslahi ya nchi.
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.