Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Dkt John Magufuli leo tarehe 25 Novemba 2019 amezindua rasmi jiwe la msingi la ujenzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa katika hafla iliyofanyika katika kijiji cha Kikombo kilichopo Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma.
Akizungumza mbele ya Amiri Jeshi Mkuu na hadhira iliokuwepo, Jenerali Venus Mabeyo alitoa shukrani zake za dhati kwa Mh. Rais kwa kukubali wito na kutenga muda wa kujumuika na Maafisa, Askari pamoja na Wananchi katika uzinduzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa. Aidha alimwomba Mh. Rais baadhi ya maeneo ambayo bado hayajamilikishwa na yana umuhimu kiutendaji yamilikishwe na JWTZ pia ameomba deni la nyumba zisizopungua 6600 zilizojengwa na kampuni ya China lilipwe na serikali.
Nae Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi alitoa shukrani zake za dhati kwa Mh. Rais kwa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha JWTZ linapiga hatua katika nyanja mbalimbali na kulifanya kuwa jeshi la kisasa zaidi. Pia aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kujitolea kuwa bega kwa bega kuunga mkono jitihada za serikali katika kuimarisha Ulinzi na Usalama nchini.
Aidha Amiri Jeshi Mkuu amewapongeza Maafisa na Askari kwa kulijengea heshima JWTZ ndani na nje ya nchi hivyo kuipa sifa Taifa letu. Katika kutatua changamoto hizo zinazoikabili JWTZ Mh. Rais Dkt John Magufuli alitoa maagizo ya kuwa askari wote wanaoishi katika nyumba hizo wasikatwe hizo fedha na badala yake deni hilo litabebwa na serikali sambamba na kutoa kibali maeneo ambayo hayamilikiwi na jeshi yamilikiwe rasmi, kuhusu barabara alimwagiza Mh.Waziri wa uchukuzi kuanza kufanya tathmini ya ujenzi wa barabara hiyo yenye umbali usiopungua kilometa 18 uanze mara moja .
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.