Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan amezindua hospitali ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) iliyofadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Jeshi la nchi hiyo (GAFTAG) iliyojengwa maalum kwa ajili ya magonjwa ya milipuko na yasiyoambukiza Lugalo jijini Dar es salaam.
Aidha, Rais Samia amepongeza uongozi wa JWTZ chini ya Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Venance Mabeyo kwa kujituma na kulinda mipaka ya nchi kikamilifu sambamba na kuitangaza nchi kimataifa kwa kushiriki ulinzi wa amani katika mataifa mbalimbali. Vilevile, amesema kituo hicho cha kipekee kimekuja wakati muafaka na kulitaka JWTZ likitunze kwa maslahi ya Taifa.
Kwa upande wake Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Mabeyo amesema mradi huu unaenda sambamba na miradi mingine ya JWTZ iliyotekelezwa kwa msaada wa Jeshi na Serikali ya Ujerumani.
Jenerali Mabeyo ameitaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni pamoja na Karakana ya magari iliyopo Lugalo jijini Dar es Salaam, Hospitali zaJeshi za Kanda na Kituo cha Ulinzi wa Amani.
Naye Balozi wa Ujerumani nchini Bi Regina Hess amesema lengo la mradi huu ni kuliwezesha JWTZ kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza. Aidha amesema, Serikali ya Ujerumani inategemea kukamilisha mradi mwingine mkubwa wa hospitali jijini Dodoma.
Uzinduzi wa hospitali hiyo yenye majengo na vifaa vyenye uboraimehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. George Simbachawene, Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Mnyepe, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Amos Makala, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Godwin Gondwe pamoja na Wakuu wa Matawi wa JWTZ.
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.