Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania linapenda kutoa taarifa ya ufunguzi wa mashindano ya kombe la Mkuu wa Majeshi (CDF CUP) ambayo yanatarajiwa kuanza rasmi tarehe 26 Mei 2017 katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam. Mgeni rasmi katika ufunguzi huo anatarajia kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe .
Mashindano haya yalianzishwa rasmi mwaka 2014. Awali JWTZ lilikuwa likiteua Wanamichezo wa kushiriki michezo ya kimataifa kupitia timu teule za Jeshi, hali iliyopelekea kutovumbuliwa kwa vipaji vipya katika michezo. Kwa muktadha huo ilionekana upo umuhimu wa kubadili mfumo wa uteuzi na hivyo kutolewa maelekezo ya kuanzisha mashindano ya Kombe la Mkuu wa Majeshi (CDF CUP), ambayo huanzia ngazi za vikosi hadi kufikia ngazi za brigedi.
Lengo la mashindano haya ni kudumisha mshikamano, kuvumbua na kukuza vipaji, pia mashindano hayo yanatumika katika kuteua kombaini ya timu ya JWTZ inayowakilisha Jeshi na Taifa kwa ujumla katika mashindano ya michezo ya Majeshi na utamaduni kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa mwaka huu 2017, mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika nchini Burundi mwezi wa nane.
Kauli Mbiu ya mashindano haya ni, “Tushiriki Michezo kama sehemu ya Kazi, Kulinda Afya zetu na kudumisha mshikamano”. Michezo ni furaha na zaidi michezo inakuza nidhamu pamoja na kujenga afya ya mwili na akili kwa Wanajeshi.
Timu zinazoshiriki mashindano haya ni Ngome (Makao Makuu JWTZ), Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Kamandi ya Jeshi la Anga, Kamandi ya Jeshi la Wanamaji pamoja na Jeshi la Kujenga Taifa(JKT).
Mashindano haya yatahusisha michezo ifuatayo; Mpira wa miguu kwa Wanaume, Mpira wa kikapu kwa Wanaume, Mpira wa mikono kwa Wanaume, Mpira wa pete kwa Wanawake, Mpira wa wavu kwa Wanawake na Mbio za nyika kwa Wanaume na Wanawake. Michezo hii itafanyika katika Viwanja vya Twalipo vilivyopo Mgulani pamoja na Uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.
Aidha, Mashindano haya yanatarajiwa kufungwa rasmi tarehe 06 Juni 2017. Mgeni rasmi katika ufungaji wa mashindano hayo atajulikana baadaye.
Hakuna kiingilio
Wote mnakaribishwa.
Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.