Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) ameweka rasmi jiwe la msingi katika uzinduzi wa Ujenzi wa Hospitali Kuu ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania inayojengwa Msalato Dodoma tukio lililofanyika Alhamisi tarehe 10 Feb 22.
Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi, Mhe. Waziri alipongeza maono ya viongozi wakiongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan katika suala la umuhimu wa ujenzi wa Hospitali hiyo ambayo itatoa huduma kwa Maafisa, Askari na familia zao pamoja na wananchi kwa ujumla.
Naye Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu alisema kuwa mradi wa ujenzi wa Hospitali Kuu ya Jeshi utaingizwa kwenye Bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023, kwa upande wa vifaa tiba kwani kukamilika kwa Hospitali kutaisaidia Serikali katika kutoa huduma za Afya kwa wananchi.
Akimwakilisha Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania Luteni Jenerali Mathew Mkingule amesema kuwa kukamilika kwa Hospitali hiyo kutasaidia kutoa huduma kwa Maafisa na Askari, kwani itakua na uwezo wa kuhudumia wagonjwa wa kutibiwa na kuondoka wasiopungua elfu moja kwa siku.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu (Mb), Balozi wa Ujerumani nchini Mhe. Regina Hess, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Bunge Mhe. Vita Kawawa, baadhi ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Majenerali, Maafisa na Askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.
Ujenzi wa Hospitali hiyo umefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Jeshi la nchi hiyo, ambapo tayari wamekamilisha miradi mbalimbali ya Hospitali kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania ikiwemo Hospitali za Kanda zilizopo Arusha, Zanzibar na Hospitali ya Lugalo Jijini Dar es Salaam.Tanzania People's Defence Forces,
P.O.Box 194 Dodoma,
Street : Miyuji, Msalato
Fax : +255 26 2962123
Tel : +255 737 962 064
E-mail : ulinzimagazine@tpdf.mil.tz
Haki zote zimehifadhiwa. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.